CHADEMA YAIBUKIA SEIKALI SAKATA LA MAKINIKIA.

Image result for tundu lissu
Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu


Timothy Marko
Chama cha Chadema kimeibuka na kutaja sababu ya ukimya wa sakata la Makinikia baina ya serikali na kampuni ya Acacia Mining PLC , pamoja na kuchelewa kuwasili nchini ndege moja iliyonunuliwa na serikali aina ya Bombardier,  iliyotarajiwa kuingia mwishoni mwa mwezi Julai mwaka huu.
Wakati akizungumza na wanahabari leo Agosti 18, 2017 jijini Dar es Salaam, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu amedai kuwa ukimya wa serikali kuhusu sakata la Makinikia, umetokana na Kampuni ya Acacia kufungua kesi katika mahakama ya kimataifa ya usuluhishi ikidai fidia ya dola za kimarekani milioni 2, kama hasara iliyopata kutokana na hatua ya serikali kuzuia makontena yake yenye makinikia kusafirishwa nje ya nchi kwa ajili ya kuuzwa.
“…huko tunakoelekea hali ya nchi yetu itakua mbaya sana, niseme mengine yanayokuja, sababu ya kubadili sheria tatu na kukatisha mkataba, kampuni ya Acacia imefungua kesi katika mahakama ya usuluhishi ikidai dola milioni 2 kama fidia ya hasara iliyoingia wakati mchanga wa dhahabu ulipokamatwa,” amesema na kuongeza.
“Pia Kampuni ya AngloGold Ashanti, mmliki wa mgodi wa dhahabu Geita, kwa sababu ya kubadili sheria harakaraka, imetoa taarifa rasmi ya kutushitaki. Wanakwenda mahakamani ili kudai fidia kwa kila hasara wanayopata sababu yakubadili mikataba. Nilisema tunaenda kunyolewa mahakamani. Na taarifa tulizo nazo, makampuni mengine ya uwekezaji katika sekta ya mafuta na gesi yameanzisha mchakato wa kufungua mashitaka katika mahakama za kimataifa dhidi ya Tanzania.”
Kuhusu kuchelewa kuwasili ndege, Lissu amedai kwamba ndege hiyo imezuiliwa kutokana na utekelezaji wa hukumu mbili zilizotolewa na mahakama ya kimataifa ya usuluhishi, ikiwemo amri ya kukamatwa kwa mali za Tanzania kufuatia kampuni ya ujenzi ya Stirling Civil Engineering  kushinda kesi iliyofungua mahakamani hapo, ya kudai fidia ya deni Bilioni 87, baada ya serikali kuvunja mkataba wake wa ujenzi wa Barabara miaka kadhaa iliyopita.
“ Hadi sasa ndege haijawasili na serikali imepata kimya cha ghafla. Miaka ya nyuma kampuni ya Stirling ilivunjiwa mkataba wake wa ujenzi wa barabara na kufungua kesi mahakamani, mahakama iliamuru serikali ilipe fedha baada ya kushindwa katika kesi. Licha ya jitihada mbalimbali za kulipwa deni lake, hadi sasa serikali haijalipa,” amesema.
Lissu amedai kuwa,hasara hii siyo mara kwanza kwa nchi kubebeshwa mzigo wa madeni yanayotokana na maamuzi ya kukurupuka ya mawaziri na viongozi wa ngazi za juu. Huku akirejea baadhi ya kesi za madai zilizowahi kufunguliwa dhidi ya serikali, ikiweo ya kampuni ya Sea Tawariq ikitaka fidia ya bilioni 6 kufuatia meli yake ya samaki kukamatwa na serikali.
Mwanasheria huyo wa Chadema amedai kuwa, kufuatia hasara hizo, Bunge, vyama vya siasa na wananchi wanatakiwa kuishinikiza serikali kuweka hadharani kesi zote zilizofunguliwa dhidi ya nchi, katika mahakama za kimataifa za usuluhishi ili wananchi wafahamu gharama na hasara inayoingia taifa.
“Gharama ya serikali kufanya maamuzi ya kukurupuka bila kuzingatia mikataba na masharti yake iliyosaini na wawekezaji ni kubwa, kama hivi nilivyozungumzia na anayesema tusiogope kushitakiwa na gharama, huyo mtu anaitakia nchi balaa na anapaswa kuzomewa na kila mtanzia nayeipenda nchi yake. Anayefanya maamuzi haya ukishtakiwa unafilisika, hapo ndipo tumefikishwa,” amesema na kuongeza.
“katiba yetu imetoa majibu,  imesema, rais anapofanya makosa ya aina hii anapaswa kuwajibishwa, katiba imesema rais anapofanya makosa haya anapaswa kuwajibishwa na bunge kwa kushitakiwa na kuondolewa madarakani, na katiba imesema rais akiondolewa na bunge na kinga ya mashitaka ya jinai inaondolewa.”
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chadema, amedai kuwa “taifa lolote huongozwa na katiba yake na sheria, tunapopuuza sheria moja kwa moja tunapuuza mikataba yetu, mtawala wa nchi anapofikiri yuko juu ya mkataba mwisho wa siku wanaoathirika ni wananchi na si yeye, kauli za kiongozi wa taifa ni za msingi pale ambapo zinatolewa kulingana na katiba, sheria na mikataba tunayoingia. Mikata inapokuwa na dosari zipo taratibu za kisheria za kurekebisha kasoro.”

Comments

Popular posts from this blog

Mvua yatatiza mpambano kati ya Simba SC na El Masri

Marubani Wawili Wapoteza Maisha kwa Ajali ya Ndege Zanzibar

TANZANIA KUWA MWENYEJI WA CHANGAMOTO ZA MADAWATI YAKIJINSIA JUNE 13